Sunday, November 22, 2009

Viagra ya wanawake yagunduliwa!

0 comments


Wataalamu wamegundua bila kutarajia Viagra ya wanawake, wakati walipokuwa wakifanya uchunguzi wa dawa ya kuondoa mfadhaiko wa mawazo au antidepressant. Katika majaribio matatu tofauti, imeonekana kuwa dawa iitwayo flibanserin ina athari ya ajabu katika kuongeza nguvu za kufanya mapenzi kwa wanawake, bila dawa hiyo kuwa na athari yoyote katika kuondoa mfadhaiko wa fikra. 

Wanasayansi hao wa Chuo Kikuu cha Carolina Kaskazini nchini Marekani wamesema kuwa, katika chunguzi huo usiokuwa wa kutarajiwa, imeonekena kuwa dawa hiyo inaongeza nguvu za kujamiina kwa wanyama wa maabara na binaadamu pia. Wamesema kuwa, ni muhimu kupatikana dawa kama Viagra kwa wanawake, kwani itatumiaka kutibu kutokuwa na matamanio ya kufanya mapenzi au libido kitaalamu, ambayo ni moja ya matatizo sugu ya kijinsia waliyonayo wanawake.

Monday, November 16, 2009

Uamuzi wa kutoa au kuacha mimba – Part 2

0 comments

Katika makala iliyopita, niliandika mlolongo wa hadithi 12 za ukweli nilizowahi kuambiwa na baadhi ya wanawake waliowahi kuwa na mimba, zilitokea bila kutarajiwa au kupangwa.

Bila shaka unaweza ukaongezea nyingine zinazohusiana na kuwa na mimba bila kutegemea, kwani mwenye mimba ya aina hii huisi inaingilia maisha, shughuli, mategemeo au kazi zake.

Mimba imekuwa kero, imeleta shida, wasiwasi, mzozo, usumbufu na taabu, kwa Kiingereza zinaitwa ‘inconvinience’.

Katika makala hii, tuangalie wanawake wa aina hii, wataamua vipi kuendelea kulea mimba na kuzaa au kutoa mimba.

Katika hali hii wapo ambao hadithi zao nilizoelezea wataiacha mimba ikue na kuzaa mtoto.

Siyo kwamba wao mimba haiwapi shida, usumbufu, wasiwasi, mzozo, kero na taabu, ni kwamba wameamua kwa sababu limetokea.

Wameamua ingawa mimba itabadilisha maisha yao na hata uhusiano. Japo ni kero, shida, wasiwasi, mzozo, usumbufu, taabu lakini watairuhusu hiyo mimba iendelee na watajifungua.

Wanaona kuwa mimba si mwisho wa dunia. watasema “Liwalo na liwe, mimba nitalea, mtoto nitazaa”. Suala la kuitoa mimba haliwaingii kabisa kichwani.

Wana msimamo kama mgombea urais wa Chama cha Republican huko Marekani na ilani ya uchaguzi wa chama hicho inayosema kuwa kutoa mimba ni shambulio la kuua kiumbe hai kisicho na hatia na hakina ulinzi.  

Wengine wataamua kuitoa, hawa walioamua kutoa mimba kila mmoja ana sababu zake. Kuna wanaodai wanataka waendelee na masomo, wengine wanawaogopa baba na mama zao, jumuiya itamuonaje, mume wake atamuua pengine bosi atamfukuza kazi ama jamii itajua, maana ni mtu mkubwa nchini, anakwepa aibu na kufikiria jinsi gani waumini watamwona kwa kuwa ni kiongozi wa kanisa ama mchungaji. 

Sababu hizi ni nyingi na zinatofautiana lakini zote unaweza ukazijumlisha kwa maneno matatu ya Kizungu, ambayo ni ‘convinience’, expediency’, ease. Ikimaanisha utoaji mimba unaleta utulivu, utakuwa poa, utaleta faraja, utatulia, utamaliza mahangaiko, kero, shida, wasiwasi, mzozo, usumbufu na taabu.

Kama kina mama na kina dada hawa wakiamua kuitoa hiyo mimba, nini sababu ya msingi na maana yake ni nini? 

Sababu na kusudi la msingi ni kumaliza taabu, mzozo, shida, kero wanavyosema Wazungu ‘The end justifies the means’ yaani, fanya lolote mradi umetimiza azima yako na lengo lako la kutoa kero, aibu, usumbufu. 

Kwa hiyo kila mmoja na mimba yake ameishaamua afanyeje, kuna makundi mawili.

Moja limeamua kuilea mimba na kuzaa, hili tuliite ‘K’ maana yake kuzaa na kundi jingine wameamua kuitoa, hili tuliite ‘A’ maana yake (abortion).

 Kundi la kwanza ‘K’ yaani walioamua kuilea na kuzaa linagawanyika na kuwa makundi mawili, la kwanza ni wale tangu mwanzo waliamua kuilea. Hili tuliite ‘K1’. Suala la kuitoa halikuwaingia akilini.

Kundi la pili ‘K2’, limefikiria kuitoa lakini baadaye likaaamua kuilea japo lilikuwa linafikiria kuitoa au kutoitoa.

Tofauti kati ya ‘K1’ na ‘K2’ ni kwamba ‘K1’ hakufikiria kuwa kuna njia mbili, alijua kuwa njia ni moja tu, kuzaa na kulea. ‘K2’ alifikiria kuna njia mbili, kuzaa na kutoa mimba na mwisho kuamua kuilea na kuzaa.

Kwenye kundi (A) ambalo limeamua kuitoa kuna makundi mawili (A1 na A2). A1 ni wale ambao walifikiria kuitoa au kutoitoa na mwisho kuamua kuitoa. A2 ni wale ambao hawakufikiria kuitoa au kutoitoa na walipojua kuwa wana mimba walienda moja kwa moja kuitoa.

Kwao kutoa mimba ni kama kunywa maji pale unaposikia kiu. Anahisi ana mimba, moja kwa moja anaenda kuitoa.

Katika kufikia uamuzi wa kuitoa na kutoitoa bila shaka kila mmoja kwa kujua au kutojua, kwa kusudia au kutokusudia kulikuwa na mambo yaliyokuwa yakimwongoza kichwani mwake.

Kwa kundi la kwanza K1 ambalo pamoja na kero, usumbufu, matatizo na mengineyo, wameamua kuilea mimba bila hata kufikiria, kuitoa ni utu wao, dhamira au labda dini yao.

Kwa jinsi wasivyoweza kufikiria kutoa mimba, wao wanafikiri utoaji mimba ni kuua. Wana msimamo juu ya kuheshimu miili yao, wanajua katika kutoa mimba, mtoaji anagusagusa, anawaingia kwa kutumia vyombo sehemu ya miili yao.

Wazo hilo kwa hali walivyo na utu, kibinadamu wanaona haiwezekani. “Wacha hayo matatizo, kero na usumbufu viendelee lakini siwezi nikaua kiumbe changu tumboni, sitaki mtu aniguse mwili wangu, aniingie mwilini na hasa pahala nyeti,” wanasikika kwa nyakati tofauti wakisema watu hao.

Kuna ambao uamuzi wa kutotoa unatokana na woga wa kudhurika wakati wanapoitoa kwani wameishasikia na hata kuona vifo, taabu, kutozaa na matatizo mengi yatokanayo na utoaji mimba.

“Wacha tu nilee hii mimba nisije kufa nikiitoa, nisije nikawa tasa, nitoke damu nyingi hata kuongezewa damu na ndugu wote wajue kuwa nimetoa mimba, nisije nikachanika vibaya ndani na nje.

“...Nimeishasikia kuwa kunatokea hata kizazi kupasuka unapotoa mimba na kusababisha upasuliwe tumbo lote kutoa kizazi na baada ya hapo huzai tena.

“...Nasikia unaweza ukafa, juzi tu kwenye magazeti msichana wa miaka 16 amepoteza maisha wakati akitoa mimba huko Arusha,” wanasema.

Wanaoamua kuitoa bila hata kufikiri huenda wakawa na matatizo, wengine labda wameishatoa au wameona rafiki zao walitoa na wako salama kama yule mtoto wa kidato cha nne ambaye mdogo wake yupo kidato cha kwanza ana mimba.

Wengine wameishasikia wenzao wakitoa mimba na wako salama na shida ziliisha. Huyu mtoto wa kidato cha kwanza alishasikia kuwa dada yake mkubwa wa kidato cha nne ametoa mimba na sasa anamaliza masomo.

La msingi ni kuwa wanaotoa wanafikiri kufanya hivyo kutamaliza kero, shida, matatizo na tabu.

Uamuzi wa kutoa au kutotoa mimba ni wa mtu binafsi, hata kama kuna mtu labda marafiki au mume mnaomshauri na kumshawishi mtu atoe au ailee uamuzi wa mwisho ni wake.

Katika kufanya uamuzi ni vizuri mtu akawa na habari na hata takwimu fulani zinazomsaidia kuamua kufanya au kutofanya hivyo.

Uamuzi wa kuacha, kutoa mimba – 1

0 comments

KUNA usemi usemao mtu anajifunza kutokana na yanayomtokea yeye mwenyewe au yanayowatokea watu wengine.

Hebu angalia na uone kama unaweza ukajifunza kutokana na visa hivi kumi na mbili vilivyowatokea mabinti na akina mama ambao walipata mimba bila kutegemea na labda kulikuwa na uwezekano wa kuzitoa hizo mimba.

Unajua utoaji mimba ni suala muhimu sana likigusia mtu binafsi, familia, elimu, afya, uchumi na hata siasa.

Umeona jinsi misimamo tofauti katika utoaji mimba kati ya Barack Obama wa Chama cha Democratic na John McCaine wa chama cha Republican ilivyowachanganya wapiga kura huko Marekani na kuwa suala muhimu katika kuamua wampe nani kura zao.

Mfano, msichana anayesoma amekwenda likizo na huko amekutana na rafiki wake wa kiume, na baada ya muda akawa anajisikia dalili za mimba. Hajaona siku zake za mwezi, asubuhi huwa anajisikia kichefuchefu na wakati mwingine hutapika na huwa anachokachoka.

Matiti yake yamekuwa mazito halafu yameongezeka ukubwa na anaona katika chuchu zake weusi umezidi. Anajisikia kwenda haja ndogo mara kwa mara. Hizi ni dalili za mimba na baada ya miezi mitatu tumbo litaanza kuwa kubwa na ataonekana kabisa ana ujauzito.

Atafukuzwa shule, baba na mama ni wakali na huenda wakamfukuza nyumbani aende kuishi na bibi kijijini! Sasa afanyeje?

Mimi niko chuo kikuu, ni msichana ambaye nimejiweka katika hali nzuri kabisa. Sikuwahi kutembea na wanaume (kufanya ngono) miaka tangu nizaliwe. Walionisaidia kujiweka salama ni wazazi wangu, kwani walikuwa wananiangalia hata kunichunga.

“Usiongee na mvulana yule...ni mhuni, hata baba yake ni mhuni. Ukitoka nijue unakoenda na unaenda na nani? Kumbuka saa 11 jioni uwe umerudi, ikifika saa 12 kama hujarudi, ole wako,” walisema wazazi wangu.

Nilifikiri wazazi walikuwa wananionea na mimi niliwajibu. “Mbona Farida wazazi wake wanamruhusu hata hadi saa 4 usiku.”

Nilipokuwa chuoni hapakuwa na wa kunilinda, kunichunga wala kunilazimisha. Nilijitangazia uhuru! lakini sasa najuta. Nina mimba na huu ni mwaka wa kwanza tangu niingie chuoni. Wazazi nitawaambiaje? Hii degree nitaimaliza lini? Wenzangu wataniacha nyuma. Kwanza hata mwanafunzi mwenzangu aliyenipa mimba ameniambia hana mpango tena na mimi. Nifanyeje?

Msichana ana mchumba na wamekusudia kuoana miezi miwili ijayo lakini msichana hajatulia. Anafanya mipango ya kuaganaagana na rafiki zake wengine wa kiume, maana akishaolewa ndiyo mwisho tena. Sasa ana mimba na akimwambia mchumba wake atajua anambambikizia, kwani mchumba huyu ni mtu mwadilifu na hafanyi tendo la ndoa ovyo ovyo.

Akiolewa na mimba atakapozaa mume akifanya hesabu atajua tu alioa mke mwenye mimba ambayo siyo yake! Afanyeje?

Mimi ni mwanamke niliyeolewa lakini sijatulia, sasa nina mimba. Hatujapanga kabisa na mume wangu kuzaa mtoto mwingine sasa. Nitamwambia kuwa ilikuwa bahati mbaya! wiki ile tulipokutana sikuchukua tahadhari.

Hata hivyo, nina uhakika atajua, atakugundua tu. Akigundua ataniua. Unajua pamoja na kuelimishwa kwa kina baba kuwa waache kutupiga na kutunyanyasa, bado kabisa hawajaelimika! Nifanyeje?

Mimi msichana nimetafuta sana nafasi ya kwenda kusoma ng’ambo, sasa nimeishaipata na nina mdhamini ambaye ni serikali. Ni nafasi yangu ya kujikwamua kimaisha, kiuchumi na kifamilia, nitaenda Marekani nitarudi na digrii yangu, baadaye nitachukua PhD. Nitaitwa daktari. Nitaweza hata kuwa profesa kama Profesa Anna Tibaijuka.

Sasa nina mimba, nisipochukua nafasi hii ya kwenda kusoma, nikiiachia haitarudi tena. Nifanyeje?

Mume na mke wamezaa mtoto wa kwanza, mama ananyonyesha na mtoto ana miezi mitano tu. Mama anajisikia kama ana mimba, walikutana wakati siku za mwezi hazijarudi na hawakuchukua tahadhari. Mama anaenda hospitali kupima kama ana mimba, mtoto anayemnyonyesha ana miezi mitano tu, sasa ana mimba. Watu watamuonaje? Na huko kazini watamuelewaje? Maana ni juzi tu amerejea kazini baada ya likizo ya uzazi.

Sheria ya kazi hainiruhusu kwenda likizo ya uzazi tena mapema kama ambavyo imetokea kwangu. Wanasema hadi ipite miaka mitatu, kwani nimeshindwa kumpata hata msichana wa kazi wa kumlea huyu mtoto. Nikienda kazini narudi mapema kumchukua kwa jirani na kumnyonyesha, maziwa yenyewe hata sina! Maziwa ya kopo ni ghali, Nitafanyaje?

Mimi ni msanii na mwanamitindo, wanaume wananifuatafuata sana, hili si kosa lao na si kosa langu. Mimi nimeumbwa mzuri, uzuri wangu unaoniweka mjini na hata ukinipeleka nje ya nchi nitakubalika pia.

Hapa nina mimba, siwezi kunengua au kunyatanyata tena kwenye jukwaa. Siwezi kuyavaa yale mavazi ya kuonyesha maungo na uzuri wangu ili kujipatia kipato.

Ninaweza nikailea hii mimba na kuzaa lakini baada ya kuzaa mwili wangu utakuwa umebadilika, utakuwa hauna soko tena wakati ndio unaoniweka hapa mjini! Nitafanya nini baada ya kuzaa?

Mimi na mme wangu tuko kwenye ndoa, tumezaa watoto watano, kuwalea, kuwasomesha, malazi na chakula ni kitendawili lakini tunaendelea hivyo hivyo na mradi maisha.

Hatuwezi kuongeza mtoto mmoja zaidi ya kulisha na sale za shule. Sasa nina mimba ya miezi miwili. Nitafanyeje? Mimi ni mtu mkubwa kwenye nchi hii, naonekana mara kwa mara kwenye runinga na magazetini. Nina cheo kikubwa, nyumba ndogo wangu ana mimba.

Familia yangu itajua, wananchi watajua na Waandishi wa magazeti, wakijua habari hizi. Oh! nitakataa lakini siku hizi kuna vipimo vya DNA ambavyo vinathibitisha baba wa mtoto ni nani. Nifanyeje?

Mimi ni kiongozi wa dini, sijui limenijia shetani gani lakini huyu muumini wangu niliyekuwa namwongoza kimaisha, kindoa na kiroho ana mimba yangu.

Sikumbuki kama ni mimi niliyempa kishawishi au ni yeye aliyenishawishi lakini ukweli yote haya yalikuwa kazi ya ibilisi. Kwanza mke akijua, washiriki wakijua. Mume wake akijua, mkuu wangu wa dini akijua kuwa kondoo alionikabidhi nichunge nimewala badala ya kuwachunga. Nitafanyaje?

Nilivyoipata kazi yangu hii hapa ofisini ni siri yangu, unajua tena sisi tumeingia darasani lakini hatukusoma. Cheti cha kuingia chuo kikuu tuligushi na mitihani ilikuwa ya kuibia na hata kuajiri waliokuwa na akili zaidi yangu kunifanyia mitihani.

Nilikuwa na wahonga hata mabwana zangu kwa njia ninayojua mimi wanifanyie mitihani, lakini mwisho nilifanikiwa nikahitimu ila siyo kiwango cha kuweza kupata kazi. Ukiniambia kuwa nilipata hii kazi kwa hongo ya ngono unanidhalilisha lakini niko hapa kwa kuwa bosi na mimi tunaelewana hasa baada ya kazi. Nina mimba ambayo siyo ya bosi huyu, atakapogundua kibarua tena hakuna. Nifanyeje?

Mimi nimeingia kidato cha kwanza mwaka huu, nimetoka kijijini kwetu huko Morogoro ndani ndani, kwenye shule niliyokuwa nasoma mimi tu ndiye niliyefaulu nikiwa msichana.

Wenzangu hawakufaulu, wameishia kulima kijijini na wengine wameenda mjini kufanya kazi za ndani na biashara ndogo ndogo za mitaani. Baba, kaka, mama na dada zangu wamekuwa wakiuza mihogo na karanga wanazolima kugharamia masomo yangu, sare za shule na sanduku la kuweka nguo alininunulia bibi yangu baada ya kuuza mtama.

Hapa shuleni kuna wasichana wawili walio kidato cha kwanza na cha nne. Walikuwa wakinitoa kunipeleka kwa rafiki zao na mimi nikapata rafiki. Tulikuwa tunawatembea hao marafiki siku za Jumapili tunapopata ruhusa na hata mara nyingine siku za kazi baada ya kumpa mlinzi fedha kidogo.

Nilipo hapa nina mimba, nashangaa wenzangu wako salama lakini mimi mdogo ndiye tayari. Hata hivyo huyu mmoja wa kidato cha nne alishatoa mimba mara moja, mimi ndiyo tegemeo ya baadaye maana katika familia k kwani kati ya watoto sita tuliozaliwa na baba na mama mimi tu ndiye niliyefanikiwa kwenda kidato cha kwanza. Nifanyeje?

Kina mama na dada hawa 12 wanafanana kwa njia mbili, kwanza wamepata mimba bila kutarajia au kupanga. Pili mimba imekuwa ni kero, shida na tabu.
Blog Widget by LinkWithin